Sunday, November 27, 2016

ANTONY LUSEKELO(MZEE WA UPAKO): WACHUNGAJI NA MANABII WOTE WALIONIPIGIA SIMU KUNIPA POLE KWA KILICHOTOKEA NI "WAPUMBAVU">>>>>

MCHUNGAJI ANTONY LUSEKELO(MZEE WA UPAKO)
MCHUNGAJI wa Kanisa la Maombezi (GRC), Anthony Lusekelo maarufu kwa jina la Mzee wa Upako, amewajia juu na kuwaita wapumbavu, manabii na wachungaji waliompigia simu kumpa pole baada ya kudaiwa kutishia kuua walinzi wa jirani yake na taarifa hizo kuandikwa katika vyombo mbalimbali vya habari.
Mzee wa Upako ameyatoa maneno hayo jana jumapili tarehe 27 November 2016 wakati wa Ibada ya Jumapili katika kanisa lake hilo lililopo Ubungo – Kibangu(river-side) jijini Dar huku waumini wake wakiwa na shauku ya kujua kilichotokea lakini hakuingia kwa undani zaidi ya kutupa lawama kwa maadui zake.
“Mwaka huu niliahidi kusamehe wote hivyo nimewasamehe. Kama siaminiki mimi, basi iaminini kazi yangu, hakuna nabii ambaye hajapitia haya ninayopitia.
“Nawaambia manabii na wachungaji walionipigia simu kunipa pole ni wapumbavu. Ukiwa bondia, basi ukubali manundu,” amesema Mzee wa Upako akiwa madhabauni kwake na kusema kwa kifupi kilichotokea:
“Kilichotokea mimi nilikuwa narudi nyumbani kwangu majira ya saa 10 jioni, nikakutana na vijana wawili, wa kiume na kike, nikaanza kuwauliza maana ninakoishi ni kama tunaishi mashetani, sina jirani, kila mtu ana maisha yake, utasikia tu sauti ya geti asubuhi mtu anatoka na jioni anarudi.
Sina jirani, hivyo nikawauliza wale vijana mnakwenda wapi maana tunakoishi hakuna watu wengi na wengi wao wana magari yao. Nilikuwa nina haki ya kuwauliza kwani hata ile barabara nimejenga mimi mwenyewe. Ni kama walikuwa wametumwa vile, cha ajabu wakaanza kunitukana na mimi kama mwanadamu nilishikwa na hasira..., wakakimbilia kwa jirani ambaye ni mzungu. Lakini yaliyoandikwa wanajua wenyewe,walioandika sisi tufanye kazi ya Injili.
“Vijana wa Kamanda Sirro (Kanda Maalum ya Dar es Salaam) wananishika na kunidhalilisha lakini mimi sitishiki wala sikati tamaa ilimradi sina kosa hata Yesu alishikwa. Kama kuna mtu anamfahamu nabii au mtume ambaye hajapitia majaribu ambayo mimi nayapitia anitajie.
“Nimepokea simu nyingi sana za manabii na wachungaji, ooooh! Mzee wa Upako imekuwaje, nikawatukana pumbavu maana ni tusi la neno katika Biblia. Nimegundua kwamba kumbe nakubalika, haijalishi ni kwa mabaya au mazuri, magazeti, tv na media mbalimbali kwa jumla nimewekwa front page. Kumbe ninauza. Lakini kwa nini hawaandiki mazuri ninayoyafanya? kama mwanamke niliyemuahidi mtoto ndani ya mwaka huu na amepata mtoto. Kwa mwaka huu niliahidi kusamehe hivyo nimewasamehe wote.”
Mchungaji huyo amesema hasingezungumza kwa undani kama ambavyo wengi walidhani lakini amewaomba waumini wake wasubiri baada ya mwezi mmoja kuisha.
Akihubiri wakati wa ibada hiyo, Mzee wa Upako amewasifu waumini wake kwa kufurika kanisani kuliko siku nyingine yoyote tangu mwaka huu umeanza.
 
 
 

No comments:

Post a Comment